21/05/2026
WIZARA YA UJENZI : SERIKALI KUJENGA ZAIDI YA KILOMETA 1,495 KWA KIWANGO CHA BARABARA YA LAMI HADI KUFIKIA 2026/31.
Dodoma.
Waziri wa Ujenzi, Mhe. Abdallah Ulega (mb) amesema Serikali ya Awamu ya Sita (6) inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan inatarajia kujenga Kilometa 1,494.45 kiwango cha Lami na Madaraja makubwa 18 kwa miaka mitano (5) wakati akiwasilisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara hiyo kwa Mwaka wa Fedha wa 2026/2027, hatua itakayoimarisha miundombinu ya Sekta ya Usafirishaji kuwa fungamanishi na kuchochea ukuaji wa Uchumi.
Mhe. Ulega amesema, Mtandao wa Barabara za Kitaifa (Road tarmac) unaoratibiwa na Wakala wa Barabara TANROADS umefikia Kilometa 37,734.41 ambapo Kilometa 12,225.26 zimeshajengwa kwa kiwango cha lami. Aidha, Amefafanua wakati Tanzania inapata uhuru mwaka 1961 nchi nzima ilikuwa na Kilometa 1,360 pekee kwa Barabara za kiwango cha lami, huku Serikali ya Awamu ya Kwanza (1) mpaka Awamu ya Tano (5) zikijenga jumla ya Kilometa 9,369.81. Hali inayoonesha Kasi kubwa ya Maendeleo ya Miundombinu katika Ukanda wa Afrika Mashariki ikiwa ni Mafanikio yanayoendelea kutekelezwa na kushuhudiwa na Serikali ya Awamu ya Sita (6) nchini.
Aidha , amebainisha kuwa Katika Utekelezaji wa Bajeti ya Mwaka 2025/2026 Wizara ya Ujenzi ilipanga kujenga na kukarabati Kilometa 450 za Barabara kuu na Mikoa za Kilometa 820 kwa kiwango cha lami na Changarawe. Hadi kufikia Aprili 2026, Serikali ilikuwa imeshakamilisha ujenzi na ukarabati wa Barabara za Kiwango cha Lami za Kilometa 94.36 za changarawe. Pia, Serikali imeeleza kuwa Utekelezaji huo unafungamana na ongezeko la Juhudi na Ubora wa miundombinu ya Usafiri ili kukidhi mahitaji ya wananchi kwa kurahisisha na kuharakisha ukuaji wa shughuli za kiuchumi.
Kwa upande wa Ujenzi wa Miundombinu ya Madaraja , Mhe. Ulega amebainisha kuwa Serikali imekwisha kamilisha jumla ya ujenzi wa Madaraja Tisa (9) ikiwemo Mitomoni (Ruvuma), Mirimba (Katavi) , Nzali (Dodoma) , Kaleba (Kagera) na Itembe (Simiyu) na ujenzi wa madaraja 11 unaendelea huku Serikali ikiandaa miradi mipya ya madaraja 13 ikiambatana na Upembuzi Yakinifu na Usanifu wa miradi mbalimbali. Aidha, Serikali imesisitiza miradi hiyo ni sehemu ya utekelezaji wa mkakati wa uimarishaji miundombinu ya Kisasa na kuongeza fursa za ukuaji wa uchumi wa ndani ya nchi kwa kurahisisha shuguli za kijamii na kiuchumi nchini.