31/12/2025
SAFARI YA DEBORA
MWANAMKE WA AJABU SOKONI
Debora alionekana akitembea katikati ya barabara iendayo jiji la kijani kibichi, kwa hatua za kujiamini kana kwamba ardhi aliyokanyaga ilikuwa imeshazoea ndoto zake. Mbele yake lilisimama gari kubwa aina ya wanteni ya kisasa, liking’aa chini ya jua la asubuhi kana kwamba nalo lilitaka kushuhudia hadithi yake.
Kila aliyemwona Debora alibaki na swali moja moyoni:
“Ni mwanamke wa aina gani huyu?”
Alikuwa ametoka kwenye soko kubwa la mazao ya shambani, soko lililojaa sauti za wauzaji, harufu ya matunda mabichi, na ndoto za watu wanaotafuta kesho bora. Kijana mmoja aliyejulikana kwa jina la Gatu, baada ya kumwona Debora mara kadhaa sokoni hapo, aliona haiwezekani kuendelea kupita kimya kimya.
Alimsogelea kwa adabu akamsalimia.
“Samahani dada, naona mara kwa mara unakuja hapa. Naomba nifahamu, nini hasa kinakuleta sokoni kila siku?”
Debora alitabasamu—tabasamu lenye fumbo, tabasamu la mtu aliyepitia mengi lakini hakupoteza tumaini.
“Mimi ni mkulima na mfanyabiashara wa mazao ya shambani,” alimjibu kwa sauti tulivu.
Maneno yale yalimshangaza Gatu.
Mkulima? Na gari k**a hili?
Akakumbuka methali ya wahenga: “Usimdharau mtu kwa muonekano, hujui alipotoka wala aendako.”
Gatu alitamani kuuliza mengi zaidi, lakini Debora alimkatisha kwa upole.
“Kama unataka kunifahamu zaidi, njoo mashambani kwangu kijijini Mtokambali.”
Kabla hajapata jibu, Debora alikuwa tayari amepanda gari lake na kuondoka, akimuacha Gatu amesimama na mawazo mazito kuliko mzigo wa gunia la mahindi.
NDOTO YA GATU
Usiku ule haukuwa wa usingizi kwa Gatu. Mawazo yalimsongamana kichwani k**a soko la mnada. Alijiuliza kwa nini yeye, kijana aliyemaliza masomo, bado alikuwa akingoja ajira ya serikali k**a mvua ya masika, ilihali Debora—mdogo kwake—alikuwa ameshajenga ufalme wa mazao.
Gatu alikuwa miongoni mwa vijana waliokulia katika imani kwamba:
“Ukisoma, ajira itakuja yenyewe.”
Lakini maisha yalikuwa yakimfundisha somo tofauti.
Aliwakumbuka marafiki zake waliokwenda nje ya nchi kwa ufadhili. Kila alipoona picha zao mitandaoni, moyo wake ulijaa wivu na maswali. Lakini sasa, kukutana na Debora kulianza kubadilisha mwelekeo wa fikra zake.
“Asiyejaribu, hawezi kujua,” alijisemea kimoyomoyo.
Siku ya Nanenane ilipofika, Gatu alitembelea soko la wakulima. Alishangazwa na kuona bidhaa nyingi zikiwa na nembo ile ile aliyokuwa ameiona kwenye kadi ya Debora. Ndipo alipokutana na rafiki yake wa zamani, Fasta, aliyekuwa sasa mshirika wa Debora katika kilimo cha mahindi na tikiti maji.
Gatu alimuliza swali Fasta, umewezaje kuwa mshirika wa karibu wa Debora?
Fasta kajibu kwa kusema kuwa,
“Debora alininyanyua kutoka sifuri,” Fasta alisema kwa fahari.
“Alinionyesha kuwa kusubiri ajira ni sawa na kusubiri kivuli cha mti usiopandwa.”
Maneno yale yalipandikiza mbegu mpya moyoni mwa Gatu.
Alijua safari yake haikuwa tena ya ndoto, bali ya maamuzi pia alitamani sana kumjua Debora hata kwa uchache kupitia Fasta.
Fasta unaweza nieleza kidogo historia ya Debora k**a unamfahamu vyema?
Ndio namfahamu vyema bosi wangu,ngoja nikueleze kwa uchache historia ya bosi Debora naona unashahuku ya kujifunza kutoka kwake. Inaendelea.............