20/02/2026
Halmashauri ya Wilaya ya Chalinze imefanikiwa kufikia asilimia 64.88 ya lengo la ukusanyaji wa mapato ya ndani kwa mwaka wa fedha 2025/26 hadi kufikia Desemba 2025.
Akizungumza wakati wa kuwasilisha makisio ya mpango na bajeti ya mwaka wa fedha 2026/27 katika kikao cha Kamati ya Ushauri ya Wilaya, Afisa Mipango wa halmashauri hiyo, Ndugu Bilali, amesema Halmashauri iliidhinishiwa kukusanya jumla ya shilingi 22,243,578,000 kutoka katika vyanzo vya mapato ya ndani.
Aidha Bilali amesema kuwa hadi kufikia Desemba 2025, Halmashauri ilikuwa imekusanya shilingi 14,432,648,867.45, sawa na asilimia 64.88 ya lengo la mwaka.
Kwa mujibu wa Afisa Mipango amesema miongoni mwa vyanzo vya mapato vilivyochangia mafanikio hayo ni kodi ya ukumbi, ushuru wa mawe, kokoto, mchanga na kifusi, ada za maegesho ya malori, adhabu na tozo mbalimbali, vibali vya ngoma na sherehe, pamoja na matangazo ya redio.
Vile vile amebainisha kuwa Halmashauri inaendelea kuimarisha mikakati ya ukusanyaji wa mapato ili kuhakikisha lengo lililobaki linafikiwa kabla ya mwisho wa mwaka wa fedha.
Kikao hicho kimefanyika katika ukumbi wa mikutano uliopo katika ofisi za Halmashauri ya Wilaya ya Chalinze na kilihudhuriwa na wadau kutoka taasisi mbalimbali za umma na binafsi