09/05/2017
SAFARI ISIYOSAHAULIKA.
Sehemu ya V.
Nilichukua pikipiki kwa safari nyingine kutoka Stendi Mpya hadi Mwandiga usiku ule! Tulitembea takribani dakika tano tu kulipofika mitaa ya Kahabwa ndipo historia yangu na dereva yule wa pikipiki aliyekuwa akijulikana k**a Mack zilipobadilika kabisa.
"Nini kile mbele bro!" aliniuliza Mack huku akipunguza mwendo kwa haraka sana.
Ndipo na mimi nikatazama mbele kwa makini... "Mungu wangu tumekufa!"
Sasa endelea......
*****
Gari kubwa lililokuwa limefunga barabara kwa juhudi kubwa zilizofanywa na matingo wa magari yaliyokuwa yamekwama pale zilizaa matunda kwa kulizamua na kufanya safari kurejea k**a kawaida. Mama Jane alikuwa ni mmoja wa abiria waliolala pale usiku wa jana yake kungojea basi lao liweze kupita. "Sijui Mathias jana walifika wao" aliwaza mama Jane baada ya kuanza tena safari yao. Ilikuwa saa nne asubuhi wakiwa wameanza kusafiri tena. Safari hii kidogo ilitia matimaini kwa sababu hali ya anga ilikuwa shwari kabisa. Saa saba mchana walifanikiwa kuwasili Kigoma na basi lao la Adventure na kushusha mzigo aliokuwa nao na kutafuta usafiri wa kuelekea nyumbani.
*****
Wote wawili Mathias na Mack walipoteza fahamu na hawakuwa tena katika ulimwengu huu. Safari yao ya pikipiki baada ya kufika maeneo yale hakuna awezaye kueleza nini kilitokea. Katikati ya umati mkubwa sana wa viumbe ambavyo haikuwa rahisi kuvitambua kwa haraka Mathias na Mack walikuwa katikati huku wakihema kwa mchoko wa mwendo wa kilometa nyingi walizotembea. Ilisikika tamko huyo mrudisheni kwa sauti iliyokuwa ya ngurumo kuu. Iliyovunjavunja miamba na kupeperusha matawi ya miti minene duniani. Mathias hakuwa tena na dereva wake alijiona pekee huku fahamu zake zikiwa kawaida lakini mwenye hofu iliyojaa mwili wake wote!
Hakujua yuko wapi na amefikaje anachokumbuka alikuwa kwenye pikipiki na alikuwa anaelekea nyumbani usiku ule! Umati ule wa viumbe vya ajabu na kutisha uliendelea kuongezeka zaidi na zaidi huku ikiashiria kufanyika kwa kikao kikubwa sana ambacho ajenda zake hakuzijua muda ule.
Mathias alijiwazisha huku akitetema mwili wote ukiwa umelowa jasho. Muda wote yanafanyika hayo Mathias hakujua ni mchana au usiku! Hakuhisi njaa, kiu, wala haja yoyote kiasi ambacho hakuelewa. Wakati huo fikra zake zikikuwa kawaida kabisa k**a mtu anayeona yote yaendeleayo ingawa akili ilianza kupoteza kumbukumbu muda baada ya muda. Kilichomshangaza zaidi na kumpa mawazo aliyotaman kujua...pale yupo wapi? ...na kwanini? Alikosa majibu.
Akafumba macho yake yaliyokuwa yamelowa kwa kutiririkiwa kwa jasho akapoteza fahamu!
Mukajaga!!.....Mukajaga!!..... Mukajaga!!.... Iyoooh!!.... Iyoooh!!.... Nyimbo ziliimbwa kwa sauti kuu iliyomfanya Mathias azinduke ghafla. Alistaajabu kuona umati ule wa viumbe kwa hesabu ya harakaharaka ni watu wote wa dunia hii mara kumi na tano wakutanike mahali pamoja yaani sehemu k**a ukumbi. Viumbe vile viliendelea kuimba na kucheza kwa kutikisa masingo ya vichwa vyao. Vilifurahi sana! Mathias alipepesa macho yake huku na huko kwa hofu na woga wa ajabu sana.
Viumbe vyote viliketi na kufanyiza hadhara kuu ambayo Mathias hakuwa na jeuri tena hofu, woga, wasiwasi vyote vililindima ndani ya mwili wake. Muda wote hayo yakitokea alikuwa amelala mahali ambapo muda wote alipigwa na vitu k**a mawimbi yaliyomfanya masikio yake kuanza kupoteza uwezo wa kusikia vizuri. Halikuwa amelala juu ya vitu vilivyokuwa lojolojo k**a maji.
Baada ya umati ule kuketi sauti ya ilisikika ikiamrisha Mathias abebwe apelekwe mbele kabisa. Viumbe takribani milioni hamsini vilinyanyuka na kumtwaa Mathias juujuu na kumsogeza mbele.
*****
Mama Jane aliwasiri nyumbani salama salimini na kulakiwa na mwanae wa pekee Jane.
"Waaaooh.... Mama yangu...!!" Jane alimkimbilia mama yake na kumkumbatia kwa nguvu. Alifurahi sana kufika salama kwa mama yake kutokana na misukosuko aliyokuwa akimueleza wakati wote wa safari yake.
"Hamjambo hapa!" mama Jane aliuza huku akivua sweta na kuagiza aletewe maji ya kunywa ya baridi. Jane aliingia ndani na kuleta maji kwa mama yake.
"Ebu nenda pale sokoni kwa Hassan uone k**a mzigo wangu umemalizika kushushwa maana nineacha wanashusha" alimuagiza Jane na bila hata kuongeza neno akaelekea sokoni kuuangalia mzigo wa mama yake.
Akiwa anakunywa maji mawazo ya Mathias yalimjia na kuamua ampigie simu ili kujua k**a na yeye jana alifika salama.
"Mteja unayempigia hapatikani kwa sasa. Tutamtaarifu kwa sms atakapokuwa hewani!"
"Atakuwa ameishiwa moto!" alijisemea na kunyanyuka akaingia ndani na kuelekea chumbani kwake akavua nguo zake za safari akajifunga kanga kifuani akatoka nje na akaingia bafuni kuoga walau kuondoa machovu ya safari ya siku mbili njiani.
Jane punde akarudi na kumkuta mama yake amemaliza tayari kuoga na kutenga chakula wale pamoja.
"Ulikuwa hujala tu? "
"Ndio nilikusubili ufike kwanza"
"Sawa! Leta apa nje tu"
Wakaanza kula huko wakiongea mawili matatu mama na mwana!
"Alafu mama kuna mkaka kapotea ghafla na alikuwa yupo safarini wametangaza msikitini Shia" Jane alimwambia mama yake.
"Amepotea? Alikuwa ametokea wapi? " "Walisema Kahama"
"Mmmh ni hatari!"
"Alikuwa anaitwa Mathias kijana mwenyewe! " aliongeza Jane.
Mama yake akashtuka ghafla... "Mathiasss???"
"Unamjua mama!"
"Mungu wangu! Atakuwa anepatwa na nini huyu. Nimempigia sasa ivi simu yake na haipatikani. Nilikuwa nae basi moja na tuliongea sana hadi tukapeana namba. Jana yeye walitangulia na basi jingine!"......
Mama Jane hakuendelea tena kula akachukua simu yake na kuipigia namba ya Mathias. Akajibiwa vilevile k**a awali. Akapumua kwa nguvu akaingia chumbani. Jane hakuelewa chochote!
*****
Mukajaga ni sehemu ambayo katika vitabu vingi vya masimulizi ya kutisha palisimuliwa na watu wengi sana. Kila hadithi yake iliposimuliwa kila mtu alijawa na hofu na wasiwasi nyakati za usiku wakati wa kulala. Kitu hasa kilichokuwa kunaogofya ni namna ya mahali hapo maisha yake yaliyo ya kutisha yaliyojaa mauaji mengi ya haraiki ya mamilioni kwa mamilioni ya watu wake. Hakukuwa na kitu kinachoitwa haki za raia. Hakukuwa na kitu kinachoitwa mahak**a ili haki itafutwe hapo. Kila kitu na amri ilitoka kwa 'Fute'. Huyu ndiye mungu wa mahali hapa.
Huabudiwa na kutukuzwa.
Yeye ndiye mwanzo na mwisho.
Akisema amesema.
Akikataa amekataa.
Hufanyi lolote bila yeye kujua.
Ole wako awe na hasi yoyote na wewe ndiyo unakuwa mwisho wako.... Kifo ndio haki pekee anayesitahili yeyote nchini hapa.
Picha na ramani ya nchi hii inamkanganyiko mkubwa, huwezi kuipata katika fikra za kibinadamu. Pande zote nne zipo na mipaka yote ipo lakini nchi zote jirani hazina majina yanayozitambulisha. Hazitamkiki. Hazifikiki na wala haziishiki.
Mukajaga ilikuwa ya pekee.
Ukifika umefika.
Ukitoka umekufa.
Na ukifa binadamu huomboleza kwa vilio na machozi ya majonzi ya kupoteza wapendwa wao! Hadithi hizi ndizo ziliwafanya wengi kusisimka na kupatwa na hisia kali za wasiwasi. Hakukuwa na historia ya mwanadamu yeyote kufika huko. Mtu pekee aliyefanikiwa kufika yasemekana alifika huko kabla hajazaliwa na alikuwa ni mtoto wa mzee mmoja maarufu miaka mingi sana hata kabla ya wakoloni wa Kijerumani. Mzee huyo alijulikana kwa jina ya Nziza na aliishi zaidi ya miaka mia, mitaa ambayo sasa inaitwa Kisitwe. Binti Ndiyu alikuwa mke wa saba wa mzee Nziza. Alikuwa ndiye mke wa mwisho katika orodha ya wake zake.
Yalikuwa ni majira ya mvua nyingi alipobeba ujauzito wake wa kwanza. Ujauzito uliendelea kukua na afya yake ilikuwa njema isiyo na shaka yoyote. Miezi tisa iliwadia na mabadiliko ya uchungu ikiwa ni dalili za kujifungua alipata. Kwa kuwa ulikuwa ni ujauzito wake wa kwanza ilibidi wake wenzake wamuangalie kwa huduma na maandalizi ya kujifungua.
Muda ya jioni wingu lilitanda likiashiria kunyesha kwa mvua muda wowote. Binti Ndiyu akiwa amejilaza chumbani kwenye nyumba yake alianza kujisikia uchungu sana. Tumbo la uchungu lilimkata na hakuona msaada mwingine zaidi ya kumwita mke mwenzake mama Shala ambaye walitazama nyumba. Muda huo huo mvua nayo ilianza kunyesha kwa kasi huku ikiambatana na radi na ngurumo za hapa na pale. Mama Shala aliwaita wake wenzake tayari kujiandaa na kumsaidia mwenzao ajifungue salama. Uchungu uliendelea! Uchungu ukashika kasi!
Binti wa watu akajitupa huku na kule!
Akajinyonga akajipindua weee.... Uchungu ukawa uchungu....
Binti akasukuma na kusukuma lakini wapi....
Siku ikapita hali ikapoa...
Ujauzito upo palepale.
Hakuna aliyeelewa kilichotokea.
Siku zikasonga.... Miezi kumi na mbili ikatimia. Ujauzito wa Binti Ndiyu anafanikiwa kujifungua mtoto wa kiume. Hakuna aliyeamini kuzaliwa kwa mtoto yule. Akapewa jina la kiha la Kahitila yaani aliyevuka muda. Kahitila akaendelea kukua na kukua. Akiwa na umri wa karibu miaka miwili Kahitila alipotea ghafla katika mazingira ambayo hakuna anayejua chochote kuhusu yeye mpaka leo! Hapo ndipo jina la Mukajaga ilipotajwa na mzee mmoja mashuhuri katika uganga na utabiri pale kijijini. Hakuendelea zaidi kulitaja jina hapo wala kutoa habari zake kwa hofu za matendo ya mahali penyewe. Watu walibaki na taharuki.
Huyo ndiye mtu aliyetajwa kuwa alienda na akarudi ingawa alienda hajazaliwa yaani kile kipindi cha kupitiliza kwa ujauzito wake na kuondoka kwa kupotea wakati ambao hajaanza kuongea hata sentensi!
Mathias alikuwa Mugajaga.... Iliyotajwa vizazi na vizazi kwa hadithi ileile iliyoogofya karne na karne.
Itaendelea.......
Maoni na ushauri.
Email : [email protected]
WhatApp 0757536278.